advanced Search
KAGUA
7181
Tarehe ya kuingizwa: 2012/11/11
Summary Maswali
Vipi mtu anaweza kuwa kipenzi cha Mwenye Ezi Mungu?
SWALI
Vipi mtu anaweza kuwa kipenzi cha Mwenye Ezi Mungu?
MUKHTASARI WA JAWABU
Katika lugha ya Kiarabu, -ambayo ndiyo lugha ya sheria ya Kiislamu- neno (pendo) linatokana na neno "حب". Ambalo lina maana ya kule mtu kuwa na mapenzi na mtu, kitu au jambo fulani. Lakini neno pendo, mapenzi au neno jengine lenye maana kama hii, linapotumika na kunasibishwa na Mwenye Ezi Mungu, huwa halina maana na uelewa wa mapenzi ya kibinadamu. Kwani mapenzi ya viumbe yanatokana na sinikizo la uathirikaji wa nasfi zao, kutokana na hali za kimaumbile walizoumbika nazo, jambo ambalo Mola Mtukufu ametakasika nalo. Penzi la Mola kwa waja wake linatokana na yeye mwenyewe kuwa na mapenzi na dhati yake. Yeye ni mwenye kuyapenda matendo yake, na kwa kuwa viumbe vyake vyatokana na matendo yake, hivyo basi yeye pia ni mwenye kuvipenda viumbe vyake.
  Kuna njia tofauti zenye kumpelekea mja kupendwa na Mola wake, kama lilivyobainishwa jambo hilo ndani ya Qur-ani, pale Mola alipozitaja sifa za wapenzi wake. Miongoni mwa sifa alizozitaja Mola Mtukufu katika Qur-ani ni; kuwa na subira, kuwa na taqwa (uchamungu), kutubia, kuwa na hisani, usafi wa tohara ya mwili pamoja na moyo, na pia ikiwemo jihadi katika kusimamisha dini yake. Hivyo basi, mwanadamu akishikamana na sifa hizo ataingia katika kivuli cha mapenzi ya Mola wake.
JAWABU KWA UFAFANUZI
Katika lugha ya Kiarabu, -ambayo ndiyo lugha ya sheria ya Kiislamu- neno (pendo) linatokana na neno "حب". Ambalo lina maana kuwa na mapenzi na mtu, kitu au jambo fulani, au kuwepo kwa fungamano la dhati baina ya nafsi moja na kitu, mtu au jambo fulani. Neno hili pia lina maana ya kuvutika na kitu, mtu au jambo fulani, kiasi ya kwamba mtu hujihisi kutokuwa na stahamala ya kutengana na kile anachokipenda au alichofungamana nacho.
Pendo la Mola kwa waja wake
 Pendo au mapenzi ni sifa maalumu iliyo thibitifu (iliyo thibiti na kujikita), na moja kati ya sababu za kuwepo kwake, ni kule mwenye sifa hiyo -yeye mwenyewe- kujipenda dhati yake, hali ambayo kila mmoja huwa nayo.
Mola ni mwenye kujielewa pamoja na ni kuuelewa ukamilifu wake ipaswavyo, jambo ambalo humpelekea yeye kujipenda. Vile vile penzi hilo la kuipenda dhati na ukamilifu wake, hupelekea kuwapenda viumbe wake wote (wanyama, wanadamu, majini na malaika) pamoja na kila alichokiumba, kwani vyote hivyo vyatokana na utendaji wa matendo yake yeye mwenyewe.
Penzi la Mola kwa waja wake halifanani na mapezi la waja au viumbe wake wenyewe kwa wenyewe, kwani Mola ametakasika na mfumiko wa nafsi pamoja na mafungamano yake ya ndani na nje. Na iwapo atakuwa kama wao, basi naye atalazimika kuwa na mfumiko maalumu wa maumbile ya nafsi, wenye kupelekea kuwepo kwa utashi wa mambo mbalimbali, lakini Mola ametakasika na hayo.
Penzi la Mwenye Ezi Mungu linatokana na kule yeye kuipenda dhati yake. Kule Mola kuipenda dhati yake, ni sawa sawa na yeye kupenda aina zote za kheri. Pia Kule yeye kuwa na elimu juu ya uzuri alionao, hilo humfanya yeye awe ni mpezi (mwenyekupenda) dhati yake, na hapa dhati huwa ni mtenda, yaani ni mpendaji. Na kwa upande wa pili, dhati yake huwa ni yenye kutambuliwa kielimu kupitia dhati yake yeye mwenyewe, basi kwa mtazamo huu, dhati yake itakuwa ni mpendwa wa dhati yake kupitia dhati yake.
  Kwa kuwa matendo yake Mwenye Ezi Mungu (ambayo ni viumbe wake) hayapambanukani naye, na wala hayapo nje ya dhati yake, hivyo basi matendo hayo yatakuwa ndani ya kivuli cha pendo lake Subhanahu Wata’ala. Na hiyo ndiyo maana ya Mola kupenda matendo (matendwa) yake. Na kule viumbe wake kuwa ni natija ya matendo yake hayo, hivyo basi viumbe wake wote watakuwemo ndani ya pendo lake Subhanahu Wata’ala.
Ni kweli kuwa viumbe wote wamo ndani ya pendo lake Mwenye Ezi Mungu Mtukufu, lakini ndani ya makala hii twataka kufikia natija ya pendo maalumu na makhususi la Mwenye Ezi Mungu juu ya wanadamu.
  Ili ifahamike vyema, ni vipi mwanadamu ataweza kuingia ndani ya kivuli cha penzi la Mwenye Ezi Mungu? Na vipi mja huyo ataweza kufikia kilele cha upendo wa Mola wake? Kwanza ni lazima kuwatafiti na kuwatambua wapenzi wake Mola Mtukufu. Hii ni kwa ajili ya kuufikia na kuufahamu uelewa wa sifa walizonazo wapenzi hao, ili mwanadamu aweze kushikamana na sifa zao na hatimae kushikamana na njia walioshikamana nayo.
  Ndani ya Qu-rani Tukufu kuna makundi maalumu ya watu waliotajwa ndani yake, ambao wamefanikiwa kupata penzi la Mola wao. Nao ni wapezi wake Subhanahu Wata’ala. Baadhi ya makundi hayo ni kama ifuatavyo:
1- Wenye sifa ya Subira; "والله یحب الصابرین..."  {Mwenye Ezi Mungu anawapenda wenye subra (stahamala)}.[1]
2- Wenye sifa ya uchamungu; "... فان الله یحب المتقین" {Basi kwa hakika Mola anawapenda wachamungu}.[2]
3- Wenye kumtegemea Mola wao; "... ان الله یحب المتوکلین" {Hakika Mwenye Ezi Mungu anawapenda wenye kumtegemea}.[3]
4- Wenye kutubia; "... ان الله یحب التوابین و یحب المتطهرین" {Hakika Mwenye Ezi Mungu anawapenda wenye kutubia na wenye kujitakasa}.[4]
5- Watenda hisani; "... ان الله یحب المحسنین" {Hakia Mwenye Ezi Mungu anawapenda wenye kutenda hisani}.[5]
6- Wanajihadi; "ان الله یحب الذین یقاتلون فی سبیله..." {Hakika Mwenye Ezi Mungu anawapenda wenye kupigana jihadi ndani ya njia yake}.[6]
7- Watenda haki na uadilifu; "... ان الله یحب المقسطین" {Hakika Mwenye Ezi Mungu anawapenda wenye kutenda haki na uadilifu}.[7]
Hayo ndiyo makundi ya watu wenye kupendwa na Mwenye Ezi Mungu.
   Nini basi maana halisi ya mja kupendwa na Mwenye Ezi Mungu?
Maana ya Mola kumpenda mja wake ni kwamba; Mola humuondolea mapazia yaliomo moyoni mwake, ili mja huyo amuone Mola wake kupitia jicho la moyo wake. Jambo ambalo humsaidia mja huyo na kumpa uwezo wa kuzifikia daraja za juu mbele ya Mola wake. Jambo hili la Mola kumtunuku mja wake na kumpa fursa kama hii inamaanisha kuwa Mola anampenda mja huyo.
  Kwa ibara nyengine ni kwamba maana ya Penzi la Mola kwa mja wake, ni kuutakasa moyo wa mja huyo kutokana na kila kisichokuwa Yeye (Mwenye Ezi Mungu), na hatimae kikiondoa kila chenye kumtenganisha mja huyo na Mola wake katika moyo wake. Wanairfani (Waliobahatika kupata jicho la kimoyo au kiakili katika kumtambua Mola wao) wanaamini kuwa, kuna aina mbili za mapenzi ya Mola Mtukufu kwa waja wake:
1- Penzi anzilifu (msingi); ambapo kila mmoja –miongoni mwa waliopewa taufiki ya penzi hili-, huwa amepewa taufiki na rasilimali maalumu yenye kumwezeshwa yeye kumuabudu na kumtii Mola wake. Taufiki ambayo huwa ndiyo sababu msingi ya kumwezesha yeye kutenda ibada.
2- Penzi la kuchuma au penzi la kustahiki; ni tunda linalozaliwa kupitia jitihada za mja akiwa katika njia ya kumtii na kumuabudu Mola wake. Tunda ambalo huwa ni natija ya mja huyo kujipamba na sifa zipendwazo na Mola wake. Jambo ambalo huweza kupatikana kupitia njia mbili:
A- Kujikurukibisha kwa Mwenye Ezi Mungu kupitia ibada za sunna.
B- Kujikurukibisha kwa Mwenye Ezi Mungu kupitia ibada za faradhi (wajibu).
Ni jambo lililo wazi kwamba, moja kati ya dalili za mapenzi ya Mola kwa mja wake, ni kumpa taufiki ya mja wake kufanya ibada na kumuabudu yeye, kutekeleza amri zake na kuachana na makatazo yake. Dhihiriko la mapenzi ya Mola kwa waja wake ni dhihiriko la rehema zake juu yao, pamoja na takrima zake kwa kwao wao.
 
Njia za kutafuta mapenzi ya Mwenye Ezi Mungu
1- Hatua ya kwanza katika kutafuta mapezi ya Mwenye Ezi Mungu; ni kuutakasa moyo kutokana na matamanio ya dunia, pamoja na kuchukua hatua ya kuelekea kwa Mola wetu Mtukufu. Jambo hili halitafanikiwa ila kuwa kuling’oa kila aina ya penzi lisilokuwa la Mwenye Ezi Mungu ndani ya nyoyo zetu. Kwani moyo wa mwanadamu ni sawa na chombo cha maji. Chombo cha maji, bila ya kumwaga au kutoa kila kilichomo ndani yake, hutaweza kuweka aina nyengine ya maji ndani yake bila ya kutokea mchanganyiko wa viwili hivyo ndani ya chombo hicho.
    Kwa kweli Mola hakuweka zaidi ya moyo mmoja katika kifua cha mja wake. Mtume (s.a.w.w) amesema; "حب الدنیا و حب الله لایجتمعان فی قلب واحد" {Penzi la kuipenda dunia na penzi la kumpendo Mola, katu viwili hivi havitaweza kukaa ndani ya moyo mmoja}.[8] Iwapo penzi la Mola litaingia ndani ya kifua cha mja, basi Mola peke yake ndiye atakayekuwa kipenzi halisi cha mja huyo.
2- Subra na ustahamilivu; ustahamilivu juu yale yasiyokupendeza, misiba pamoja na matatizo mbali mbali, ni moja kati ya njia zinazomsogeza mja kwenye mapenzi ya Mola wake, jambo ambalo limesisitizwa mno ndani ya Sunna pamoja na Qur-ani tukufu kupitia Aya tofauti. Ndio maana wanairfani wakawahesabu wenye sifa kama hizi kuwa ni miongoni mwa wapenzi wa Mwenye Ezi Mungu.[9]  
3- Kumfuata na kushikamana naye Mtume Muhammad (s.a.w.w); Kuhusiana na suala hili Qur-ani inatwambia;
 "قل ان کنتم تحبون الله، فاتبعونی، یحببکم الله..." Sema iwapo mwambpenda Mwenye Ezi Mungu, basi nifuateni mimi, hapo Mola wenu atakupendeni.[10] Kwa ushahidi huu wa Qur-ani ni kwamba, moja kati ya njia za kutafuta mapenzi ya Mola, ni kumfuata na kushikamana naye Mtume Muhammad (s.a.w.w). Ibnu ‘Arabi kuhusiana na hili anasema; “Kule Mwenye Ezi Mungu kufungamanisha penzi lake na kumfuata Mtume Muhammad (s.a.w.w), kunatokana na yeye (s.a.w.w) kuwa ndiye kioo kamili chenye kuakisi dhihiriko la Mola duniani humu.[11]  Kwa mtazamo wa Ibnu ‘Arabi ni kwamba; haitawezekana katu mtu kupata penzi la Mwenye Ezi Mungu bila ya kumfuata na kushikamana naye Mtume Muhammad (s.a.w.w). Kwani Mtume Muhammad (s.a.w.w) ni mfuasi halisi wa amri za Mola wake, kwa hiyo Mwenye Ezi Mungu yuwapenda kumuona Mjumbe wake (s.a.w.w), pamoja na wafuasi wake -wote kwa pamoja- wakiwa wameshikamana na sifa hiyo ya ufuasi wa amri zake Subhanahu Wata’ala.
4- Jihadi na kupambana katika njia ya Mwenye Ezi Mungu; jihadi ni moja ya njia zinazomwezesha mja kufikia mapenzi ya Mola wake. Wapambanao katika nijia ya Mwenye Ezi Mungu, ni wapenzi maalumu wa Mwenye Ezi Mungu, na wana pendo lenye hadhi maalumu kutoka kwa Mola wao. Kwani wao hawaachi kutumia kila walichokuwa nacho katika jihadi na kuyasogeza mbele malengo ya Mola wao, hao huhudhuria jihadi huku wakiweka mbele roho na mali zao katika jihadi hiyo ya vita kati haki na batili, iwe ni vita vya silaha au vya kitamaduni, wao huwa siku zote huwa mbele katika kupambana na maadui wa dini. Wala hawaachi kuhifadhi thamani na matakwa ya dini ya Mola wao, wapiganaji na wanajihadi hao husimama kidete wakiwa ni kama kuta zilizosimama imara kwa ajili ya kuzuia mmomonyoko na mipasuko ndani ya njia ya haki, na huyafunga mapito mbali mbali ya shetani na vitimbi vyake. Wao hawaruhusu dini ya Mola wao kutikiswa na mtu yeyote, ndiyo maana wakawa ni wapenzi maalumu wa Mwenye Ezi Mungu.
5- Kutubia na Kurudi kwa Mwenye Ezi Mungu; kutubu, kujuta na kurudi kwa Mola Mtukufu, pamoja na kuomba himaya yake, hupelekea mja kupata mapenzi ya kutoka kwa Mola wake.
Kutubu kutokana na makosa tuliyoyatenda, hulifunga na kulifuma tena upya fundo la mapezi baina yetu na Mola mola wetu, fundo ambalo lililofunguka kupitia jeuri za makosa yetu, pia jambo hili husababisha kufunguka kwa milango ya rehema za Mola Mtukufu na kutusogeza tena katika rehema zake pekee. Kule mja muovu kumwelekea Mola wake na kumuomba rehema zake, humtoa mja huyo katika hali ya uadui aliyokuwa nayo hapo mwanzo, na kumfanya mja huyo kuwa ni kipenzi cha Mola wake.
Mwandishi wa tafsiri ya Qur-ani ijulikanayo kwa jina la Tafsiri Rahnema, anaamini ya kwamba;
 Moja kati malengo muhimu katika Qur-ani yenye kuashiria suala la mapenzi ya Mola Mtuku kwa wale wenye kujitakasa na kurudi kwa Mola wao, ni kutaka kuwapa hima waja wa Mwenye Ezi Mungu kuelekea katika mlango wa toba na kujitakasa kutokana na makosa yao.[12]
6- Hisani na kusaidia wengine; Kutoa sadaka, kufanya hisani na kusaidia wengine, hupelekea kupata mapenzi ya Mwenye Ezi Mungu, kwani Mola ni mwenye kuwapenda wenye kutoa katika njia yake.[13]
7- Imani na matendo mema; Imani na matendo mema ni njia nyengine ya kulitafuta penzi na radhi za Mwenye Ezi Mungu. Malipo na uokovu wa Mola hudhaminiwa kupitia imani na matendo mema. Hii ina maana ya kwamba, imani bila ya kufuatiwa na matendo mema, katu haitaweza kumpelekea mja kupata uokovu na malipo mazuri kutoka kwa Mola wake. Jambo hili linaonekana wazi katika Aya isemayo; "والله لا یحب الظالمین"  {Na Mwenye Ezi Mungu hawapendi wenye kudhulumu}.[14]
8- Hisani na miamala mema; hisani na miamala mema ni moja kati ya njia mbali mbali za kutafuta mapenzi ya Mwenye Ezi Mungu.[15]
9- Usafi na kujitakasa; Mola baada ya kubainisha sharti mbali mbali za ibada, kama vile udhu, kutayammam pamoja na josho la wajibu, ameendelea kusema –umuhimu wa hayo- ni kwa ajili ya wanadamu kuwa na tohara na utakaso. Mola juu ya hilo anasema;
 "... ما یرید الله لیجعل علیکم من حرج و لکن یرید لیطهرکم..." {Katu Mola Mwenye Ezi Mungu hataki kukutieni mashakani (kukupeni uzito), bali yuwataka kukutoharisheni}.[16] Ni wazi kwamba amri zenye shinikizo la lazima, pamoja na aina nyengine mbali mbali za amri zitokazo kwa Mwenye Ezi Mungu, zina malengo ya kutaka kumpa mja tohara ya kimwili pamoja na tohara ya kiroho.[17] Mwanazuoni Ayatullah Jawadi Amuli anasema; “Kule Mola kuwa anawapenda wenye subra au wenye kutawakali kwake (kumtegemea yeye) pamoja na watenda uadilifu, inatokana na Yeye kulipenda suala la kutawakkal au pia kuipenda subra. Hivyo basi kwa kutokana na Mwenye Ezi Mungu kupenda subra na tawakkul, pia humpenda wenye kutawakkal kwa kuwa mja huyo ana sifa hiyo ipendwayo na Mola wake Mtukufu.[18]
Lakini yawezekana mtu akawa na sifa nyengine zaidi ya kutawakkal au subra, sifa ambazo zikawa si zenye kumpendeza Mwenye Ezi Mungu, ila bado Mola atakuwa ni mwenye kupenda kutakkal kwake au subra yake. Iwapo mja atafanya jitihada za kutafuta mapenzi ya Mola wake kupitia njia tofauti, huku akiwa hataraji chochote juu ya hilo isipokuwa radhi za Mola wake. Basi dhati ya mja huyo itakuwa ni kipenzi cha Mwenye Ezi Mungu, kisha sifa zake na matendo yake yote yapendeza mbele ya Mola wake Mtukufu.[19]  
Endapo mja atakuwa ni kipenzi cha Mwenye Ezi Mungu, hapo kila kitu ulimwenguni humu kitajenga mapenzi na mja huyo, kwani kila kiumbe hufuata matakwa na mwelekeo wa Mola wake. Hadhi na nafasi hii ya mja kua ni kipenzi cha Mwenye Ezi Mungu, ni nafasi na daraja ya juu kabisa miongoni mwa daraja za kibinadamu. Lililo muhimu kuliko yote, si mja kumpenda Mola wake, bali ni kule mja kugeuka akawa yeye ndiye kipenzi cha Mola wako.[20]
 Pale mja atakapokuwa ni kipenzi cha Mola wake, hapo matendo yake yatakuwa ni matendo ya Mola wake, maneno yake ni maneno ya Mola wake… Matokeo (matendo) ya kiungu yataakisika kupitia mja huyo. Katika riwaya maarufu inayozungumzia suala la mja kujikaribisha kwa Mola wake kupitia nawafil (sala za sunna), Mtume (S.A.W.W) amesema; ‘Mola wangu ameniambia’;
 "ما یتقرب الی عبد من عبادی بشیء احب الی مما افتر ضت علیه و انه لیتقرب الیّ بالنافلة حتی احبه..." {Hakuna kizuri zaidi anachojikaribisha nacho kwangu mja kati ya waja wangu, zaidi ya yale niliyomfaradhishia. Na mja huyo ataendelea kunikaribia mimi kupitia Nawafil (sala za sunna), mpaka hatimaye yeye atageuka kuwa ni kipenzi changu}. Hadithi hii imeendelea kusema; {Hapo basi mimi ndiye nitakayekuwa ulimi wake, na ulimi wake huo kupitia uteremsho na fadhila maalumu za utendaji wa Mola wake, utayanena matakwa ya Mola wake. Mimi nitakuwa ndiyo jicho lake, hapo jicho lake litakuwa ndiyo akisiko la matendo yaonekanayo kupitia jicho la kibinadamu. Yaani jicho lake litaona kupitia akisiko la nuru ya Mola wake. Hii inaonesha uhakika wa ile hali ya kuendana sambamba baina ya kauli na uoni wa wapenzi wa Mwenye Ezi Mungu, na kauli na uoni wake Subhanahu Wata’ala.[21]
Ni muhimu kujua ya kwamba, Iwapo mja atampenda Mola wake, penzi la Mola wake juu ya mja huyo litakuwa ni la juu zaidi kuliko penzi la mja huyo kwa Mola wake. Kuhusiana na hilo kuna riwaya isemayo: Mtume (S.A.W.W) amesema;
"اذا احب الله عبداً عشقه و عشق علیه، فیقول عبدی انت عاشقی و محبی و انا عاشق لک و محب لک، ان اردت او لم ترد"
{Endapo Mola atampenda mja wake, basi Mola atamfanya mja huyo ampende Mola wake, na Mola atajenga mapenzi yake juu ya mja huyo, kisha atamwambia: ewe mja wangu mimi nimekuwa ni kipenzi chako, nawe umekuwa ni kipenzi changu ukitaka usitake}.
Baada ya makala hii ndefu, tumefikia natija ya kwamba; kuna njia nyingi za kujikaribisha kwa Mola Mtukufu, ikiwemo njia ya subra, toba, taqwa na nyenginezo. Na kiujumla ni kwamba, kuachana na makatazo ya Mwenye Ezi Mungu, kutekelea faradhi zake pamoja na kushikamana na sunna mbali mbali, ndiyo njia asili ya mja kuweza kujenga upendo baina yake na Mola wake.
 

[1] Aalu Imran Aya ya 146.
[2] Aalu Imran Aya ya 76.
[3] Aalu Imran Aya ya 159.
[4] Baqarah Aya 222.
[5] Baqarah Aya 195.
[6] Saffu Aya ya 4.
[7] Maidah Aya ya 42.
[8] Mizanul-hikmah/Juz 2/Uk 228.
[9] Futuhati Makkia/Juz 2/ Uk 337.
[10] Aalu Imran Aya ya 31.
[11] Kitabu Futuhati Makkia/cha Ibnu Arabi/Juz 2/ Uk 336.
[12] Tafsiri Rahnema/Juz 7/Uk 486.
[13] Tafsiri Rahnema/Juz 2/Uk 274.
[14] Aalu Imran Aya ya 57.
[15] Baqarah Aya ya 195.
[16] Maidah Aya ya 6.
[17] Kitabu/ Hikmat Ibadat/ cha Abdullah Jawad Amuli/Uk: 86-87.
[18] Kitabu/ Firat dar Qur-ani/ cha Abdullah Jawad Amuli/Juz: 12/Uk: 254.
[19] Rejea iliyopita/ Uk: 256.
[20] Rejea iliyopita/ Uk: 254.
[21] Rejea Kitabu kiitwacho Sokhane Ishq cha Fatima Tabatabai/Uk: 278.
TARJAMA YA JAWABU KATIKA LUGHA NYENGINE
MAONI
Idadi ya maoni 0
Tafadhali ingiza thamani
mfano : Yourname@YourDomane.ext
Tafadhali ingiza thamani
<< Niburute.
Tafadhali ingiza kiasi sahihi ya usalama Kanuni

MASWALI KIHOLELA

YALIYOSOMWA ZAIDI