advanced Search
KAGUA
12740
Tarehe ya kuingizwa: 2006/12/12
Summary Maswali
iwapo amri za baba zitapingana na za mama, mwana atakuwa na anawajibu gani katika hali kama hiyo?
SWALI
iwapo mama atamuamrisha mtoto wake kufanya jambo ambalo baba wa mtoto atakuwa amemkataza mwana huyo kulifanya jambo hilo, katika hali kama hiyo mwana atatakiwa afanyaje?
MUKHTASARI WA JAWABU

Miongoni mwa amri kuu alizoamriswha mja na Mola wake baada ya ile amri ya kumpwekesha Mola wake, ni kwatii wazazi wawili.

 

Kuhusiana na swali lililoulizwa hapo juu, pamoja na hali halisi iliyotajwa ndani ya swali hilo, mtu anapokuwa amekabiliwa na hali kama hiyo, yeye mwenye atajikuta kuwa amebaki njia panda, kwani ni vigumu na ni jambo lisilowezekana kuwatii wazazi wawili huku ukimridhisha kila mmoja, wakati ambao amri zao zitapokuwa ni zenye kupingana. Katika hadithi ambazo zinazungumzia haki na thamani ya wazazi wawili, tutazikuta aina mbili za masisitizo ambayo yatatufanya sisi tusiweze kutoa hukumu kwa haraka, kwani kwa upande mmoja utazikutia zile hadithi zinazotilia mkazo suala la kumtii na kumpa kipau mbele baba kuliko mama, na kwa upande mwengine kuna hadithi ambazo zinatuamuru kumpa kipau mbele zaidi mama kuliko baba. Katika hali hii linalotupasa kulifanya, ni kuzipa aina zote mbili za hadithi haki yake ipaswavyo, hivyo basi katika masuala ambayo baba atakuwa ni mhusika zaidi, huku akiwa yeye ndiye mwenye haki ya utawala kuhusiana na hilo, kama vile kumuozesha mtoto wa kike aliye bikra, hapo mwana atapaswa kumtii baba yake, lakini katika masuala ambayo hayahitajii utawala wa baba, hapo mwana anatakiwa kizipa kipau mbele zaidi amri za mama yake.

JAWABU KWA UFAFANUZI

Qur-ani tukufu baada ya kumsisitiza mja kuto mshirikisha Mola wake, vile vile imemuamuru mja huyo kuwatii na kuwafanyia hisani wazazi wake wawili. Mwanachuoni (marehemu) ajulikanaye kiumaarufu kwa jina la Tabaatabai kuhusina na hilo anasema: “moja kati ya nyadhifa muhimu zilizopewa kipau mbele baada ya kumpwekesha Mola Mtakatifu, ni kuwafanyia hisani wazazi wawili”,[1] na hakuna tofauti baina ya wazazi ambao ni Waislamu au wasiokuwa Waislamu, kwani Mola alipotuamrisha kuwatii wazazi hao, hakushurutisha kuwa wazazi hao ni lazima wawe ni Waislamu, bali amesema: “wafanyieni wazazi wenu wawili ihsani.”[2]

 

Lakini kwa ufafanuzi zaidi kuhusiana na swali hili yatupasa kufafanua zaidi kwa kusema hivi:

A- yawezekana wazazi wawili wakamuamrisha mwana wao jambo ambalo ni lenye kupingana na amri za Mola Mtakatifu, katika hali kama hiyo mwana hatowajibika kuwatii wazazi wake, bali anatakiwa kutoitii amri kama hiyo.

Qur-ani kuhusiana na hilo inatuambia hivi: “Sisi tumemuusia mwanaadamu kuwafanyia ihsani wazazi wake wawili, lakini iwapo wao watakuwa na jitihada za kukufanya wewe unishirikishe mimi (Mola wako), hapo basi epukana na amri kama hiyo.![3]

Imamu Ali (a.s) anasema: “kumtii mja juu ya suala la kumshirikisha Mola, ni jambo lisilo kubalika.”[4]

Amesema tena: “haki ya mwana juu ya wazee wake, ni kuwatii na kuwafuata wazazi hao, isipokuwa katika suala linalopingana na matakwa ya Mola (s.w).”[5]

Imamu Ridha (a.s) naye anasema: “ni wajibu wa mwana kuwafanyia hisani wazazi wake wawili, hata kama watakuwa ni washirikina, isipokuwa wewe hutakiwi kuwatii wazazi hao juu ya kumshirikisha Mola Mtakatifu.”[6]

Basi kuwatii wazazi wawili ni wajibu wa kila mmoja hata kama kuwatii huko kutakufanya wewe usiweze kuyatekeleza masuala Sunna fulani, au amri za wazazi hao zikawa ni zenye kupingana na Sunna au zikakufanya wewe utende matendo ya Makruhu. Na Mafuqahaa (Wanazuoni wakuu wa Kifiqhi) wamelitilia mkazo sana suala hilo, hadi wakasema kuwa:

1-  iwapo mzazi atamkataza mwanawe kuto funga Sunna fulani, basi ni wajibu wa mwana kuwatii wazazi wake juu ya hilo, na iwapo funga ya Suuna ya mwana itawaletea aina fulani ya maudhi wazazi wake, mwana huyo atawajibika kufutari bila ya kuitimiza funga yake.[7]

2- iwapo wazazi watamuamuru mwana kuzisali sala zake kwa jamaa, basi ni bora mwana kuchukuwa tahadhari na kupingana na amri hiyo, hivyo basi anatakiwa kuzisali sala zake kwa jamaa pamoja na kutia nia ya kujikaribisha kwa Mola wake katika tendo hilo, ili sala zake zisije kuwa na harufu ya ushirikina.[8]

3- kuisali kila sala kwa wakati wake wa mwanzo kabisa, ni Mustahabbu (ni suala lililotiliwa mkazo), lakini iwapo wazazi watamuamuru mwana wao kutenda tendo jengine la Mustahabbu ndani ya wakati huo wa mwanzo wa sala, hapo basi mwana huyo kwanza kabisa, anatakiwa kulitenda tendo hilo aliloamrishwa na wazazi wake kabla ya kuisali sala hiyo.[9]

B- baadhi ya wakati inawezekana mtoto akapokea amri yenye kupingana na amri za Mola kutoka kwa mzazi wake mmoja, na wakati huo huo akapokea amri yenye kwenda sawa na matakwa ya Mola kutoka kwa mzazi wake wa pili, katika hali kama hiyo, mwana atawajibika kuitii ile amri yenye kwenda sawa na matakwa ya Mola Mtakatifu.

C- wakati mwengine mwana anaweza kutakiwa atende tendo la Sunna kutoka kwa mzazi wake mmoja, huku mzazi wake wa pili akiwa ni mwenye kumzuia mwana huyo kutenda tendo hilo. Katika hali hii tunapaswa kusema kuwa: iwapo tendo hilo litakuwa ni lenye kufungaana na haki za utawala wa baba kama vile suala la kuolewa mtoto aliye bikra, basi ni jambo la wazi kuwa, hapo mwana atatakiwa kumtii baba yake,[10] lakini iwapo suala hilo litakuwa halifungamani na haki ya mmoja kati ya wazazi hao, hapo basi itatubidi kuzizingaitia hadithi zinazohusiana na haki za wazazi wawili. Tukiwemo katika utafiti juu ya suala hili, tutaona kuwa kuna hadithi nzito zenye kutilia mkazo suala la kumpa mama kipeo zaidi kuliko baba katika utendaji wa hisani baina yao, na miongoni mwazo, ni ile hadithi isimayo kuwa: “siku moja kuna mtu aliyekwenda kwa Mtume (s.a.w.w) na kumuuliza kuwa ni nani apaswaye kupewa kipau mbele zaidi baina ya baba na mama katika kuwafanyia hisani baina yao? Mtume (s.a.w.w) akamjibu ni mama yako, akamuuliza, kisha je? Naye (s.a.w.w) akamjibu mama yako, kisha kwa mara ya tatu akamuuliza kisha je?, Naye (s.a.w.w) akamjibu mama yako, na kwa mara ya nne akamuliza tena kisha je?, hapo Mtume (s.a.w.w) akamjibu, kisha baba yako.[11]

Lakini tukitupia macho upande wa pili kuhusiana na haki za wazazi wawili, tutazikuta zile hadithi zenye kumpa kipau mbele mzazi wa kiume, na miongoni mwazo ni kama ifuatavyo:

Kuna siku moja ambayo Mtume (s.a.w.w) aliulizwa: “wadhifa mkuu wa kuwatii wazazi wawili uliomuelemea mtu juu ya shingo yake, uko katika upande gani zaidi, wa baba au wa mama?” Naye (s.a.w.w) akajibu: “uko upande wa baba”[12]. Pia kuna ile hadithi isemayo kuwa Mtume (s.a.w.w) alisema kuwa: “Wewe pamoja mali unazozimiliki ni milki ya baba yako.”[13] Tukizingatia ujumbe uliobebwa na hadithi hizi na vipi sisi tunaweza kupata suluhu isiyokuwa na mvutano, inatubidi kusema hivi: wajibu wa kuwatii wazazi wawili katika mambo yasiyopingana na matakwa ya Mola (s.w), [14] ni suala lenye muwafaka kutoka kwa Wanazuoni wote kwa ujumla, na tukizizingatia hadithi mbali mbali tutafahamu kuwa mwana anatakiwa kumpa kipau mbele zaidi mama yake, na hii haimaanishi kuwa yeye anatakiwa kumtenga au kuto mtii baba yake.[15] Na dalili za kufanya hivyo ni kama ifuatavyo:

1- hadithi ya Mtume (s.a.w.w) iliyopita ambayo ilimpa mama fadhila mara tatu katika hisani ambayo mwana anawajibika kuwafanyia wazazi wake, huku  ikimpa baba mara moja.

2- ingawaje tuna Riwaya iliyompa uzito baba katika suala la haki juu yake, lakini tukiizingatia hadithi isemayo kuwa: “Mtume (s.a.w.w) aliulizwa kuhusiana na haki za baba akasema: “haki juu ya baba ni kumtii ndani ya maisha yake” kisha akaulizwa kuhusiana na haki za mama akasema: “Iwapo mtu atamhudumia mamaye na huduma hizo zikafikia adadi ya mchanga wa jangwani pamoja na adadi ya matonyo ya mvua, basi huduma hiyo haiwezi kufanana na hata fadhila za ile siku moja tu ya mwana huyo kuishi ndani ya tombo la mamaye (pale mama alipokuwa na mimba ya mwana huyo)””.[16]

3- roho ya mama ni nyepesi mno, na roho ya aina hii ni yenye kuhitajia upendo wa hali ya juu kabisa, kwa hiyo kumtanguliza mama kiupendo na kiutendaji, huwa ni jambo lenye kuendana sawa na hali halisi ya kimaumbile aliyonayo mama mwenyewe katika maumbile yake nyororo ya kimwili na kiroho.

Kwa hali yeyote ile, kitu ambacho tunatakiwa kukizingatia hapa ni kwamba, mtoto anatakiwa kuzitekeleza amri za mamaye na kumtukuza zaidi bila ya kumletea maudhi baba yake.

 


[1] Tarjama ya Tafsirul-Mizan, juz/13, Aya ya/ 14- 23 / Suratul- Israa.

[2] Suratu Al-An-aam Aya ya 151, vile vile Imam Sadiq anasema: “Watiini wazazi wenu, wawe wema au sio wema.” Rejea Biharul-Anwaar, juz/71, uk/56, chapa ya Wafaa Beirut.

[3] Suratu Ankabuut, Aya ya 8 na Luqumaan Aya ya 15, na mbele ya Aya hii Mola anatuamrisha tusiwatupe wazazi hao hapa duniani, bali tuwafanyie ihsani ipaswavyo.

[4] Nahjul-Balagha, hekima fupi fupi.

[5] Nahjul-Balagha, hekima fupi fupi.

[6] Biharul-Anwaar, juz/71, uk/72.

[7] Taudhihul-Masail cha Imam Khomeiny, juz/1, uk/699, suala la 1741.

[8] Taudhihul-Masail cha Imam Khomeiny, juz/1, uk/769, suala la 1406.

[9] Marhum Shahid, katika kitabu chake Al-Qawaaid amesema:

Wazazi wawili wana haki katika mambo yafuatayo: “1-safari isiyokuwa ya wajibu ni haramu iwapo wazazi watamkataza mwana wao kusafiri. 2- kuwatii wazazi wawili ni wajibu hata katika suala unalolitilia wasi wasi kulitenda, kwani kuepukana na suala hilo ni wajibu lakini pia kuwatii wazazi wako ni wajibu. 3- iwapo mtoto atakuwa akielekea kusali sala yake ndani ya wakati wa awali wa sala hiyo, papo hapo akaisikia sauti ya mzazi wake ikimuamuru jambo fulani, hapo basi atawajibikiwa kumtii mzazi wake kabla ya kusali sala hiyo. 4- iwapo wazazi wake watamkataza kwenda kusali jamaa, basi ni vizuri kutokubali amri hiyo, isipokuwa katika hali ambayo iwapo yeye atakwenda kusali jamaa basi wazazi wake watakuwa mashakani, hapo basi atawajibika kuwatii katika hali kama hiyo. 5- iwapo kutatokea jihadi ambayo na Wajibu Kifai kwake, basi wazazi wanaweza kumzuia mwana wao na kumtaka abakie nyumbani. 6- iwapo mwana atakuwa anasali sala ya Sunna, kisha akaitwa na mzazi wake, hapo mwana anatakiwa kuikata sala yake na kumsikiliza mzazi wake. 7- iwapo mwana atakatazwa kufunga funga ya Sunna na mzazi wake, hapo basi mwana anatakiwa kumtii mzazi wake juu ya hilo. Rejea kitabu Al-kawaid, juz/2, uk/47-49.

[10] Wasaailu shia, chapa ya Islaamiyya, juz/14, uk/11-120.

[11] Biharul- Anwaar cha Majlisi, juz/1, uk/257, chapa ya Jaamiatul-Mudarrisiin.

[12] Sherhe ya Wasaailu Shia cha Hurrul- Aamiliy, chapa ya Islaamiyya, juz/14, uk/112.

[13] Maanil- Akhbaar cha sheikh Saduuq, juz/1, uk/257, chapa ya Jaamiatul- Mudarrisiin.

[14] Lakini pia tusisahau kuziangatia kauli za Wanazuoni kuhusiana na suala la kuwatii wazazi wawili, na kuwa jee kuwatii wazazi wawili ni wajibu?, au wajibu wetu ni kuto waudhi wazazi hao? Wanazuoni wameyazungumzia hayo kwa upana sana, baadhi yao wanasema kuwa: “kuwatii si wajibu, lakini kuwaudhi ni haramu”, huku wakifafanua  kwa kusema kuwa: “jambo ambalo litawaudhi wazazi huku likiwa jambo hilo si la wajibu kwa mwana wa wazazi hao, mwana anatakiwa aepukane na jambo hilo, au asilifanye mbele ya wazazi wake, au awaombe ruhusa mpaka waridhika juu ya kulitenda tendo hilo, lakini si wajibu kuwatii wazazi wawili, bali kinachotakiwa ni kuto waudhi wazazi hao, kwani kuwaudhi ndiyo jambo la haramu. Rejea kitabu Istiftaat suala la223, cha Jawadi Tabriiziy chapa ya kwanza ya kitengo cha uchapishaji Suruur. Jaamiul-Masaail cha Faadhil Muhammad, juz/1, suala la 2188. Taudhihul- Masaail maraaji-i cha Imam Khomeiny, juz/2, mlango wa masuala tofauti, suala la 85, chapa ya kwanza ya Islaamiyya, uk/675.

[15] Jaamiu Shataat Fii Ajwibati Sualaat, cha mahuum Mirza Qummiy, juz/1, uk/241, yeye anasema: “ukiwa na gati gati baina ya kumtii mama au baba, huku ukiwa huna njia ya kupata suluhu basi kumtii mama kuko mble zaidi katika hali kama hiyo.

[16] Mustadrakul-Wasaail, juz/15, Riwaya ya 18014-19.

 

TARJAMA YA JAWABU KATIKA LUGHA NYENGINE
MAONI
Idadi ya maoni 0
Tafadhali ingiza thamani
mfano : Yourname@YourDomane.ext
Tafadhali ingiza thamani
<< Niburute.
Tafadhali ingiza kiasi sahihi ya usalama Kanuni

MASWALI KIHOLELA

YALIYOSOMWA ZAIDI