advanced Search
KAGUA
19701
Tarehe ya kuingizwa: 2012/05/21
Summary Maswali
nini maana ya ucha Mungu?
SWALI
naomba munifahamishe, hivi neno “taqwa” lenye maana ya ucha Mungu huwa lina maana gani? Au huu ucha Mungu ndiyo nini?
MUKHTASARI WA JAWABU

Taqwa (ucha Mungu) ni nguvu maalumu za kiroho zinazo weza kupatikana ndani ya nafsi ya mwanaadamu, nguvu ambazo huwa ni himaya maalumu inayomuwezesha yeye kujitenga na maasi. Taqwa kamili ni ile inayomfanya mtu kujiepusha na maasi yanayo eleweka na kila mmoja wetu, pamoja na kujiepusha na yale yote yanayo dhaniwa kuwa ni maasi. Taqwa ni yenye daraja na vigao mbali mbali, pia natija na matunda ya taqwa ni yenye kutafautia. Ili kuutambua ufafanuzi kamili wa swali lako, basi  tunakusihi usome jawabu kamili ya swali hili inayo fuata hapa chini.

JAWABU KWA UFAFANUZI

Neno “taqwa” ni neno la Kiarabu linalo tokana na mzizi wa neno “Wiqaayatun” na serufi ya neno hilo ni "وقی یقی وقايه", neno hili lina maana ya kule mtu kujilinda kupitia kitu au ngao fulani.[1] Na katika fani ya dini, neno hili kitaalamu, lina maana ya kule mtu kujiweza au kuimiliki nafsi yake, kunakomfanya yeye awe nje ya maasi au ajitenge na maasi.

Kwa ibara nyengine ni kwamba: taqwa ni zile nguvu maalumu ambazo hugeuka kuwa ni kipaji kilichomo ndani ya nafsi ya mwanaadamu alichojichumia mja kupitia fikra na matendo maalumu, nguvu ambazo humuezesha yeye kuimiliki nafsi yake pale anapo kutana na vishawishi au pale nafsi yake inapotaka kumuelekeza katika maasi kwa namna moja au nyengine. Taqwa iliyo kamilika, haimuezeshi tu mja kujiepusha na madhambi pamoja na yale yaliyo haramishwa, bali pia inamfanya yeye kujitenga na yale mambo yenye mashaka, ambayo ndani ya uwanja wa akili madhubuti, hudhaniwa kuwa ni mambo yasiyo takikana kutendwa.

Katika Aya na Hadithi mbali mbali, imetolewa mifano mbali mbali kuhusiana na taqwa, na miongoni mwayo ni kama ifuatavyo:

  1. Mfano wa mzigo (bahasha) au zawadi: Qur-ani imaeifananisha taqwa na mzigo wa zawadi na ikasema kuwa taqwa ndiyo zawadi bora kuliko zote, na maana ya Aya iliyo sema hivyo ni kama ifuatavyo: (Basi chukueni zawadi (mzigo) na kwa hakika zawadi (mzigo) iliyo bora kuliko yote, ni taqwa.)[2]
  2. Mfano wa nguo: Qura-ni imeifananisha Taqwa na nguo na kuihisabu nguo hiyo, kuwa ndiyo nguo bora na maridadi kabisa kwa wanaadamu.[3]
  3. Mfano wa ngome: Imamu Ali (a.s) ameifanananisha taqwa na ngome madhubuti pale aliposema:

(Enyi waja wa Mungu, taqwa ni ngome madhubuti isiyo penyeka).[4]

  1. Mfano wa kipando: kwa mara nyengine Imamu Ali (a.s), ameifananisha taqwa na kipando maridadi pale aliposema: (Taqwa ni mfano wa kipando maridadi kabisa ambacho hatamu zake ziko mkononi mwa aleye kipanda, na hashuki kwenye kipando hicho hadi kimfikishe yeye Peponi.)[5]
  2. Baadhi ya wanahekima mbali mbali, waifananisha taqwa na mtu anayepita kwenye njia iliyo jaa miba, akionekana kujilinda na kujibana kisawa sawa huku akichukua tahadhari za hali ya juu kabisa kwa ajili ya kuepukana na miba hiyo, kwani yeye ana wasi wasi asije kuchomwa na miba hiyo miguuni kwake au hata kumchania nguo yake.[6] Katika mfano huu yaeleweka wazi kuwa: taqwa haina maana ya mtu kuikimbia jamii, au kuyakimbia matatizo yaliyomo ndani ya jamii yake na kwenda kuishi porini, bali taqwa ni kule mtu kuishi ndani ya jamii huku yeye akijiepusha na matatizo ya kimaadili yaliyomo ndani ya jamii hiyo.[7]

Taqwa ni kimurimuri chenye kuashiria kuwepo kwa imani juu ya Muumba na siku ya malipo.[8]

Kwa mtazamo wa Qur-ani, taqwa ni nuru itokayo kwa Mola Mtukufu, na popote pale iangazapo nuru hiyo, basi hupatikana ongezeko la elimu na maarifa.[9]

 

Daraja mbali mbali za taqwa

Taqwa ni yenye daraja mbali mbali. Baadhi wacha Mungu wameigawa taqwa katika daraja tatu zifuatazo:

  • Kuiepusha nafsi kutokana na adhabu ya milele kupitia njia ya kuchuma imani sahihi.
  • Kujiepusha na aina zote zile za maasi iwe katika mambo ya wajibu au makatazo.
  • Mtu kuiweza na kuimiliki nafsi yeke mbele ya yele yanayoweza kuushughulisha moyo waek na kuueleka mbali na Mola wake, na hii ni daraja maalumu ya taqwa, na wenye kuhusika na taqwa hii, ni wale watu maalumu, tena ni maalumu kweli.[10]

 

Vitawi  vya taqwa

Taqwa ina aina mbali mbali za vitawi, na miongoni mwa vitawi ambavyo vinaweza kuashiriwa kirahisi kabisa, ni kama ifuatavyo: taqwa kwenye mali na uchumi, taqwa katika masuala ya kijinsia, taqwa ndani ya kijamii, taqwa ya kisiasa na taqwa katika maadili binafsi. Mwenye taqwa anatakiwa kuitumia taqwa yake binafsi katika kuyachunga mambo yote tuliyoyataja hapa.

 

Matunda ya taqwa

Taqwa ni yenye matunda mbali mbali adimu katika maisha ya binaadamu, na miongoni mwayo ni kama ifuatavyo:

  1. Kuimarisha ubinaadamu na kumjenga mwanaadamu: Imamu Ali (a.s) anasema: (Taqwa ni ustaarabu na sifa ya kiroho yenye malezi ya kiaama, na chini ya kivuli cha taqwa roho ya mwanaadamu hutengenezwa na kuleleka ipaswavyo.[11]
  2. Kuyatii majukumu na kuyatekeleza ipaswavo: asiyekimbia majukumu ya kazi au wadhifa wake, ni yule mwenye taqwa, kwani yeye ndiye mtu pekee mwenye kuyakubali majukumu yake kwa roho safi yenye upendo, na wala yeye huwa hajali ugumu au uzito unao patikana katika utekelezaji wa majukumu hayo.
  3. Uhuru: taqwa ni chombo kinachomtoa mtu katika hali zote zile za utumwa, mwenye taqwa haonekani kusalimu amri mbele ya matamanio yake ya kutaka uluwa au mengineyo, hivyo yeye haonekani kusumbuliwa na mambo yenye kuwaangamiza baadhi ya watu, mambo ambayo chanzo chake hasa, huwa kinatokana na mtu kuitii nafsi yake pasi na mipaka maalumu.
  4. Uongofu: taqwa ndiyo ufunguo wa uongofu, mja kupitia taqwa yake aliyo nayo huwa anatenda yale mema na kuuelekea uongofo wa Molawe, jambo ambalo humpa yeye saada (humueka katika furaha isiyo na majuto) duniani na Akhera, na humfanya yeye aelekee kwa Mola wake bila ya kuwa na khofu ya malipo yenye kahsara.

Hayo yote tuliyo yazungumza na kuyafafanua kwa namna mbali mbali ni mambo msingi katika mtu kupata muelekeo sahihi. Huu basi ni mlolongo wa ibara zenye maelekezo kamili kuhusiana na swali lililo ulizwa hapo juu, yaani swali juu ya maana halisi ya neno “taqwa”.


[1] Angalia neno "وقی" katika kitabu Mufradaatu-fi-Ghariibil-Qur-ani, cha Husein bin Muhammad Isfahaniy, juz/1, uk/881, chapa ya Daarul-Ilmi Damascus na Al-Daarush-Shaamiya, Beirut Lebanon.

[2] Suratul-baqara, Aya ya 197.

[3] Suratul-Aa’raaf, Aya ya 26.

[4] Nahjul-Balagha, hutuba ya 157.

[5] Nahjul-Balagha, hutuba ya 16.

[6] Raudhatul-Jinaan-wa-Ruhul-Jinaan-fi-Tafsiril-Qur-ani, cha Husein bin Ali, juz/1, uk/102, chapa ya Buniaad Pazjuuheshhaye Islaaamiy Astaane Qudsi Radhawiy, Mash-had, Iran, mwaka 1408. Tafsiri Nemune ya Nasir Makaarim Shiraziy, juz/1, uk/80, chapa ya kwanza ya Darul-Kutubil-Islaamiyya, Tehran, mwaka 1374 Shamsia.

[7] Tafsiri Nemune ya Nasir Makaarim Shiraziy, juz/22, uk/204.

[8] Suratul-Hujurati Aya ya 14.

[9] Suratul-Baqara, Aya ya 282.

[10] Tafsiri Nemune ya Nasir Makaarim Shiraziy, juz/22, uk/205. Biharul-Anwaar, cha Allaama Majlisy, juz/70, uk/136, chapa ya Alwafaa, Beirut Lebanon, mwaka 1404 Hijiria.

[11] Khutbatul-Muttaqiin, ilioko ndani ya kitabu Nahjul-Balagha.

 

TARJAMA YA JAWABU KATIKA LUGHA NYENGINE
MAONI
Idadi ya maoni 0
Tafadhali ingiza thamani
mfano : Yourname@YourDomane.ext
Tafadhali ingiza thamani
<< Niburute.
Tafadhali ingiza kiasi sahihi ya usalama Kanuni

MPANGILIO WA KIMAUDHUI

MASWALI KIHOLELA

YALIYOSOMWA ZAIDI